Pages

Sunday 4 September 2016

HOFU NI ADUI YAKO MKUBWA (SEHEMU YA 1)

Watu wengi katika dunia ya leo wameshindwa kufanikiwa ama kufikia malengo na ndoto zao kwa sababu ya hofu yakufanya kile ambacho wao huweza kuwatimizia malengo yao. Na hofu hiyoimewakosesha amani, ujasiri, na kutokujiamini juu ya masuala wanayoyahitaji katikashughuli zao kwa namna moja ama nyingine. Hofu inapotawala sana hutengeneza kushindwa. Ukiishi ndani ya msukumo wa hofu kila hatua moja utakayopiga kwenda mbele, hofu itakurudisha hatua moja au zaidi nyuma. 

Miaka ya 2007 kwenda 2008, nilikuwa napenda sana kuitazama mieleka. Mieleka ni mchezo hatari sana unaopendwa hasa na watu wa ughaibuni, ndio maana wanatoa onyo kali ya kwamba usijaribu mchezo huo, kwa sababu ni mchezo usio na utofauti na vita. Katika mieleka watu huweza kuumia vibaya, kupata ulemavu wa kudumu hata kupelekea kifo. Japo kuwa kuna hatari katika mchezo huo, watu wamekua wakiendelea kuucheza na wengine kujiunga kuucheza, ingawa onyo kali limetolewa. Kitu nilichojifunza kutoka kwa washiriki wa mchezo huo ujasiri wa kutafuta pesa na mafanikio. Kitu kingine ni nini hasa kinachowafanya waendelee kuucheza na kujiunga kushiriki mchezo huo, ni kwa sababu wamekubali kuiondoa hofu ndani yao juu ya mchezo huo hatari. 

Wacheza mieleka wanaamini ikiwa utakuwa na hofu hautaweza kushiriki katika mchezo huo na wala hautaweza kupata mafanikio. Swali la kujiuliza kama watu wameondoa hofu zao juu ya mchezo huo hatari, kwanini hofu ikuzuie wewe kufanya kile unachotaka kukifanya ili kutimiza ndoto zako? Hofu ni zile hisia za ndani kabisa ambazo hutujaza hali ya wasiwasi, mashaka, mfadhaiko, woga au utisho juu ya jambo Fulani. Hofu ni matokea ya mtu kujiona huwezi, haujikubali na hauna uhakika wa mambo unayoyafanya. Kitu kinawatofautisha watu waliofanikiwa na wasiofanikiwa ni namna ya kukabiliana na hofu. 

Duniani kote hakuna mtu aliyeweza kufanikiwa kwa kuogopa hofu, iwapo mtu akishindwa kuhimili kuishinda hofu basi hatoweza kufanikiwa.  Yatupasa kufahamu kuwa hofu hutengenezwa na mazingira uliyonayo au unayoishi, na baadae huingia ndani ya mtu taratibu kisha kukua hadi kukomaa. Hofu ikikomaa ni hatari zaidi. Hofu sio kitu halisi cha kuhofia, watu wamekua wakihofia hofu bila kuifahamu hofu ikoje. Kama nilivyosema hapo awali kuwa hofu hujazwa na kutokujiamini, kujikubali, kuogopa kutenda jambo Fulani. Hofu ni picha tu, inayomtokea mtu anapotaka kutenda japo Fulani kwa mfano. Unataka kuwa mwandishi wa vitabu, inakujia picha (hofu) kwa uwezo wako huu mdogo ni nani atapoteza muda wake kusoma vitabu vyako? Je utawezaje kuwachukua wasomaji na kuwavutia kusoma vitabu vyako wakati wamezoea kusoma vitabu vya waandishi Fulani mashuhuri? Una kitu gani kipya cha kukiandika na kuwaambia watu wakati kila kitu kimeshasemwa na waandishi wengine waliopita na waliopo? 

Hiyo ndiyo hofu hujengeka kutokana na hali ya kutokujiamini na kukithamini kile ulichonacho. Kuna muda unahitaji kufanya kilimo, biashara au shughuli yoyote ile ya maslahi kwako ila hofu inakuzuia. Ikiwa utaruhusu hofu kukuingia na ukaikubali, hautaweza kuifanya shughuli hiyo na kuifanikisha. Hofu itakutengenezea picha ya kuona hasara peke yake juu ya jambo unalotaka kulifanya. 

Fahamu kuwa tabia ya hofu kwa kiasi kikubwa ni kutoa matokeo hasi. Wakati mwingine hofu inatengenezwa toka tukiwa watoto au katika mazingira tunayokulia. Hofu hizi zinajengwa na kukuzwa katika akili yetu na ndizo huleta madhara.  

Kwa mfano, watoto wengi wamasikini wamejengewa hofu ya kutojaribu au kufanya shughuli zitakazo wapa mafanikio kwa kuambiwa maneno ya kukatisha tamaa kama "maji hufuata mkondo" ikimaanisha kama wewe ni maskini utakufa maskini, kwa sababu utaishi maisha ya kimaskini waliyopita wazazi wako na ndugu. Au “unaambiwa mkono mtupu” haulambwi hii inaamisha wewe na umaskini ambao umezaliwa ndani yake huwezi kuwa na positive impact (matokeo chanya) katika jamii yako, isipokuwa wanaopaswa kufanya shughuli hizo na kuwa na positive impact ni matajiri peke yao. 

Pia kuna hofu imejengwa ndani yetu kuwa mtu hawezi kufanikiwa ikiwa atatokea mazingira duni, kwa mfano shule za kata, kutokana na mazingira yaliyopo katika shule hizo, ikiwa mtoto ataenda kusoma huko, atakuwa ametimiza wajibu wa haki ya mtoto kupata elimu na sio kupata mafanikio. 

Hofu inapojengwa hukua na kukomaa katika fikra na bongo za watoto, hivyo huwatengenezea mazingira ya kuogopa kujaribu au kufanya mambo makubwa na yenye maslahi kwao, kwa kuwa hofu imo ndani yao. Asilimia kubwa mazingira ya hofu toka utotoni na mazingira unayokulia hujengwa na wazazi wetu na watu wa karibu.  

Hofu pia hujengwa na mambo yaliyotokea, yanayotokea na ambayo hayajatokea. Katika hali ya kawaida tu, ni vigumu kuiepuka hofu, kwa sababu ni changamoto ambayo kila mmoja lazima aipitie. Unaweza ukapata hofu ya kutenda jambo fulani kwa sababu kuna ndugu, rafiki au jamaa yoyote unaemfahamu alifanya na hakufanikisha, alikwama, aliharibu, au alipata hasara. Kutokana na kuiona hali hiyo mwenyewe, unaanza kupata hofu ya kutokufanya hiko kitu (shughuli) ukihofia na wewe usije ukapata hasara kama walivyopata hasara wengine au unaweza pata hofu ya kufanya kitu fulani (jambo) kwa kuwa hujiamini kama unaweza kukifanya au haujawahi kukifanya. Maisha yako ni sawa na chombo cha usafiri na dereva wake ni wewe mwenyewe, na wala usitegemee kama kuna anaeweza kuja kuyaendesha maisha yako. 

Na ikiwa utategemea mtu mwingine ayaendeshe maisha yako, ukweli ni kwamba kuna anguko kubwa sana linalokuja kukutokea mbele yako, kwa sababu kila mtu anajukumu la kuyaendesha maisha yake na kama mtu akiendesha maisha yako hatayaendesha kama maisha yako bali ataendesha kama maisha yake, na siku itakapo tokea hayupo ndipo maisha yako yataenda mlama au kuharibika kabisa. 

Uendeshaji wa chombo cha usafiri inahitaji ujasiri wa hali ya juu ili kuweza kukiongoza chombo hicho. Haitakiwi kuwa na hofu kwa sababu ya vitu vinavyoweza kukutokea kama uharibifu wa chombo hiko, ajali ama vitu vingine vya kuogofya vinavyoweza kujitokeza. Ndivyo ilivyo katika maisha halisi kuna misukosuko, kushindwa, kuumia na vitu vingine vingi vinavyoweza kukusababishia kutoyafikia malengo yako. 

Ondoa kwanza hofu na uwe jasiri ili ukabiliane na changamoto hizo. Kama utaruhusu kuyaendesha maisha yako ukiwa umejawa na hofu ndani yako, tayari utakuwa umeshazuia kutimia kwa mafanikio yako. Unao uamuzi wa kuendesha maisha yako vile uonavyo wewe inafaa, ila usikubali hofu ikuingie wakati unayaendesha maisha yako. Hofu haishindwi kwa maneno, inahitaji kupingwa kwa utayari na na vitendo.

Imeandaliwa na;

Moses Chris Lumole

Teacher, Writer and Inspirational Speaker.

Phone: 0659230954

Email: lumolemoseschris@gmail.com©2016  


No comments:

Post a Comment